Jumamosi iliyopita, Oktoba 25, 2014
ilikuwa ni Siku ya Msanii Duniani ambayo kwa mara ya kwanza, Tanzania
iliiadhimisha siku hiyo katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar, mgeni
rasmi akiwa ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk.
Gharib Bilal.
Dr Chris Mauki na Jokate Mwegelo walikuwa washehereshaji wa tamasha hilo kwenye Ukumbi wa Mlimani City uliopo Dar es Salaam.
Siku hiyo ilipambwa na matukio kibao nyuma na mbele ya pazia, ambapo
kubwa lilikuwa ni la Jokate Mwegelo ambaye alikuwa miongoni mwa ma-mc wa
shughuli hiyo ya kitaifa, kumfagilia waziwazi msanii Nasibu Abdul
‘Diamond Platnumz’, kwamba hakuna kama yeye, Ijumaa Wikienda lilikuwa
ndani ya nyumba na kunasa matukio lukuki yaliyojiri.
SHUGHULI YAANZA
Kwa kuzingatia itifaki, ukiacha waalikwa wengine, kiongozi aliyeanza
kutimba alikuwa ni Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo,
Juma Nkamia na baadaye alifuatiwa na Dk. Bilal ambapo shughuli hiyo
ilifunguliwa rasmi.
MA-MC
Washereheshaji wa shughuli hiyo walikuwa ni Chriss Mauki na Jokate
Mwegelo ambao walifanya vizuri lakini mwanzoni kidizaini f’lani Jokate
alionekana kuwa na kigugumizi na baadaye akatengeneza vichwa vya habari
kufuatia kitendo chake cha kumsifia Diamond.
BURUDANI ZA AWALI
Katika burudani za mwanzo, kulikuwa na vikundi vya kudansi kisha ngoma
ya asili kutoka Ukerewe ikafuatia, baadaye ikaja Bendi ya Mashauzi
Classic chini ya Aisha Ramadhan ‘Isha Mashauzi’ ambayo haikuamsha kama
ilivyozoeleka.
Staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ akifanya yake.
TUZO ZAANZA KUTOLEWA
Tuzo ya kwanza kutolewa ilikuwa ni ya Msanii Aliyejitolea Maisha yake
Yote Katika Sanaa ambayo ilikwenda kwa mchora katuni mahiri aliyechora
michoro ya Tingatinga.
Tuzo ya pili ilikwenda kwa Msanii Aliyetoa Mchango Mkubwa kwa Jamii ambapo aliyeibuka kidedea ni Joseph Kanuti.
BURUDANI TENA
Baada ya tuzo hizo mbili, burudani iliendelea tena ambapo Ako Mpiluka
Band walionesha mbwembwe za kucheza na moto na kuwakosha mashabiki
waliohudhuria.
Diamond Akicheza na wanenguaji wake.
DIAMOND STEJINI
Baada ya Mpiluka Band, staa wa Bongo Fleva, Diamond Platnumz alitimba
stejini ambapo aliangusha bonge la shoo mbele ya makamu wa rais na
kushangiliwa.
Wakiendelea kucheza wimbo wa ‘Mdogomdogo’.
Huku Diamond akiimba nyimbo zake nyingi za zamani, zile zomeazomea
kama zilizotokea Fiesta zilizodaiwa kuwa ni kutoka kwa ‘Team Ali Kiba’,
zilizimwa na uwepo wa makamu wa rais aliyeonekana kumkubali msanii huyo
kwa kutingisha kichwa wakati anafanya shoo na sapoti kubwa aliyoipata
kutoka kwa Jokate aliyeimba naye Wimbo wa Nimpende Nani.
Unaweza Soma :
JOKATE: HAKUNA KAMA DIAMOND
Katika hali ambayo haikutarajiwa na wengi, Jokate alimfagilia waziwazi
Diamond na kusema hakuna msanii anayeweza kumiliki jukwaa kama yeye.Sifa
hizo alizozitoa Jokate kwa Diamond, zilisababisha ukumbi mzima ulipuke
kwa kelele hasa ukizingatia kuwa wawili hao walishawahi kuwa wapenzi ila
wakatengana na kile kinachodaiwa kuwa ni maneno ya watu.
Ukichanganya na kilichotokea kwenye Serengeti Fiesta 2014 ambapo
Diamond ‘alikula za uso’ ukilinganisha na mpinzani wake, Ali Kiba ambaye
alishangiliwa kwa nguvu, kitendo cha Jokate kumnadi Diamond jukwaani
kilizidi kutengeneza vichwa vya habari.
Unaweza Soma :
DIAMOND ASAFISHA NYOTA
Baadaye Diamond aliangusha Number One na Mdogomdogo ambazo ziliwafanya
watu wachizike hivyo kudaiwa kusafisha nyota yake iliyochafuka hivi
karibuni kwenye Tamasha la Fiesta katika Viwanja vya Leaders Club,
Kinondoni jijini Dar alipozomewa.
DK BILAL AONDOKA
Baada ya neno kutoka kwa waandaaji, Waziri Nkamia alimuaga Dk. Bilal
ambaye aliondoka ukumbini humo baada ya kukabidhi kitita cha Sh. milioni
tano kwa kila mshindi wa tuzo mbili zilizotolewa.
Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mheshimiwa Juma Nkamia akiongea na wasanii katika Siku ya Msanii.
NJENJE WAKONGA NYOYO
Baada ya Dk. Bilal kusepa, burudani iliendelea ambapo Kilimanjaro Band
‘Wananjenje’ walikamatia jukwaa na kukonga vilivyo nyoyo za wahudhuria.
Waimbaji wanaounda kundi la Yamoto Band Aslay, Becka, Bella na Maromboso wakitoa burudani.
JOKATE AKATA MAUNO
Katika shoo ya Njenje, mwimbaji wake mashuhuri, Nyota Waziri alikuwa
akitembea ukumbini kuwakatisha mauno wahudhuriaji na kuwataka wataje
mahali wanakotokea ambapo alipofika kwa Jokate, staa huyo alionesha
umahiri mkubwa wa kukata mauno huku akijinadi kwamba anatokea Songea.
KOMEDI KUTOKA NAIROBI
Kilichofuata baadaye ni Kundi la The Omonds kutoka Nairobi, Kenya
kupanda jukwaani na kuangusha komedi zilizowavunja mbavu wengi.
Baadaaye, ma-mc, Mauki na Jokate walipata nafasi ya kuzungumza
chochote kabla ya kuwakaribisha Yamoto Band waliomaliza shughuli hiyo
kwa kukamua ngoma zao kali zinazokimbiza mtaani kwa sasa.
Kwa picha zaidi angalia Uk. 8.
Imeandaliwa na Erick Evarist, Musa Mateja, Andrew Carlos, Nicolaus Trac na Dennis Mtima wa Global publishers.